ZITTO NIKO TAYARI KUFANYA KAZI na KIONGOZI YEYOTE WA CHADEMA
Zitto: Niko tayari
LICHA ya uongozi wa Chadema kutaka wanachama wa chama hicho kuacha
kumpa ushirikiano Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe, yeye amesema
yuko tayari kufanya kazi na kiongozi yeyote wa chama hicho aliye
tayari.
![](https://blogger.googleusercontent.com/img/b/R29vZ2xl/AVvXsEhY9GVV6oJayA_ypvWbYokH6Gchsjoc2lnQimSvwrSiOw8tW0Bq-LPB7pCeBWg8DXjuf_2WUkE1ELdPQX96HF3Fk_iT6883ZoDoqfWI_eL8eBOhH3JEUanR6R283jQv6gzd_WJ4v-pBm68/s1600/zitto+kabwe.jpg) |
Ziito Kabwe |
“Mimi niko tayari kufanya kazi na kiongozi yeyote wa Chadema ambaye
atakuwa tayari kufanya kazi nami, kwa sababu naamini suala hapa ni
ujenzi wa nchi yetu, ni ujenzi wa Taifa letu na naamini hata kama nina
mawazo kidogo, lakini ni kwa ajili ya kuiendeleza nchi yetu,” amesema
Zitto.
Akihojiwa jana na mtandao wa kijamii wa millardayo.com, Zitto alisema
sasa hivi kuna masuala makubwa kuhusu Katiba ya nchi na angependa
wananchi wajielekeze huko.
“Sijafurahishwa sana na kinachoendelea hivi sasa, maana yake wananchi
wameacha kujadili masuala ya msingi yanayowahusu, nasikitika kuona
vyombo vya habari ni habari za Zitto na Chadema, nashukuru jambo hili
limekwisha sasa kwa muda huu,” alisema akimaanisha mgogoro na chama
chake.
Alisisitiza kuwa bado ni mwanachama wa Chadema, licha ya Katibu Mkuu
wa Chama hicho, Dk Wilbrod Slaa, kutoa amri ya watu kumnyima
ushirikiano “lakini pale nitakapohitajika nitafanya shughuli za
Chadema, nitafanya shughuli za nchi yangu.”
Kuhusu ushindi wake wa juzi mahakamani, alisema si ushindi dhidi ya
chama, kwa sababu hawezi kushindana na chama chake, kwa kuwa kimemlea na
amekitumikia kwa muda wote, zaidi ya nusu ya umri wake.
“Kwa hiyo salamu ambazo napenda wananchi wazifahamu ni kwamba
tunahitaji kuheshimu sana demokrasia na misingi ya haki za binadamu,”
alisema.
Akizungumzia uamuzi wa Mahakama, uliotolewa na Jaji John Utamwa,
alisema utaweka utaratibu kwamba watu ambao ni wanachama wa vyama
hawataonewa, hawatadhulumiwa wala kukandamizwa na watakuwa huru kutoa
maoni yao wanapohitaji kufanya hivyo.
“Nataka niseme wazi kabisa kwa Watanzania ambao ni wanachama wa vyama
vingine, wasio na vyama na kwa wana Chadema, ushindi huu si dhidi ya
Chadema, ni wa Watanzania wote wanaopenda siasa safi na taratibu za
utawala bora zifuatwe kwenye taasisi zetu.
“Ni ushindi dhidi ya wanaotaka kukandamiza demokrasia ndani ya vyama,
ni ushindi dhidi ya wahafidhina wasiotaka mabadiliko katika vyama,”
alisema.
0 comments: